Vous êtes sur la page 1sur 1

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Dare es Salaam, 09 Septemba, 2017:Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Isdor Mpango
(Mb), ameviagiza vyombo vinavyohusika kuchukua hatua za kisheria dhidi ya kampuni ya
Williamson Diamond Ltd na wote waliohusika kuidhinisha usafirishaji wa madini ya almasi
kutoka migodi ya kampuni hiyo na kudanganya thamani halisi ya madini hayo kwa lengo la
kuisababishia hasara Serikali.

Dkt. Mpango ametoa agizo hilo leo tarehe 09 Septemba, 2017 baada ya kukagua madini ya
almasi yaliyokamatwa katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar es
Salaam yakisafirishwa kupelekwa nchini Ubelgiji.

Miongoni mwa hatua za kisheria ni pamoja na kutaifisha madini yote ya almasi yaliyokamatwa
baada ya kubainika udanganyifu wa thamani yake halisi, kuwakamata na kuwachunguza wote
waliohusika katika udanganyifu huo wakiwemo wajumbe wa bodi zilizomaliza muda wake na
wafanyakazi waliopo na waliostaafu.

Almasi hiyo ilikamatwa tarehe 31 Agosti, 2017 muda mfupi kabla ya kupakizwa kwenye ndege
ili isafirishwe kwenda nchini Ubelgiji, na ilipochunguzwa ilibainika kuwa nyaraka za kampuni
ya Williamson Diamond Ltd zimeonesha kuwa almasi hiyo ina thamani ya Dola za Marekani
Milioni 14.798 sawa na Shilingi Bilioni 33 za Tanzania wakati thamani yake halisi ni Dola za
Marekani Milioni 29.5 sawa na Shilingi Bilioni 65 za Tanzania.

Kabla ya kukagua almasi hiyo Waziri Mpango amepokea taarifa ya timu ya wataalamu
iliyofanya tathmini ya thamani halisi ya madini hayo ambapo kiongozi wa timu hiyo Prof.
Abdulkarim Mruma amesema pamoja na kubaini upotevu mkubwa wa fedha, kuna dosari
nyingine zikiwemo kukosekana kwa vifaa ya kupimia madini hayo, almasi kusafirishwa na
kuuzwa sokoni bila uwepo wa mwakilishi wa Serikali na ameshauri hatua za udhibiti huo
zifanyike katika madini yote yanayochimbwa hapa nchini.

Pamoja na kuipongeza timu iliyofanya tathmini hiyo na vyombo vya dola vilivyokamata madini
hayo Waziri Mpango amesema Serikali itatekeleza ushauri wote uliotolewa na timu ya Prof.
Mruma na kwamba kuanzia sasa almasi inayozalishwa hapa nchini itasindikizwa na maafisa wa
Serikali hadi sokoni na inataka kuanza kupokea gawio halali kutoka mgodi huo.

Waziri Mpango ametoa maagizo hayo mbele ya viongozi wa vyombo mbalimbli wakiwemo
Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Bw. Charles Kichere, Mkurugenzi
wa Mashtaka (DPP) Bw. Biswalo Mganga, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na
Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Brigedia Jenerali John Julius Mbungo, Kamishna wa
Madini Tanzania Mhandisi Benjamin Mchwampaka na Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es
Salaam SACP - Lazaro Mambosasa.

Benny Mwaipaja
MKUU WA KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI
WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO

Vous aimerez peut-être aussi